

Kwenu mastaa wa tasnia mbalimbali Bongo, habari zenu bwana. Poleni na majukumu ya kila siku ya kulijenga taifa.
Mkitaka kujua afya yangu, mimi ni mzima, namshukuru Mungu naendelea
kutimiza majukumu yangu, likiwemo hili la kuwaandikia barua.
Nimewakumbuka leo kupitia barua, nataka kuwaambia kwamba mimi
pamoja na mashabiki wengine wa sanaa yenu tumewachoka. Tumechoka kuona
na kusikia kila siku mkifanya maigizo kwenye maisha yenu halisi.
Hivi ni kwa nini kila kukicha tunasikia mnaachana? Kwa nini hamdumu
kwenye uhusiano wa mapenzi? Kwa nini hamdumu kwenye ndoa kama
mashabiki wenu wanavyowategemea?
Penzi linapoanza kushamiri, mnalinadi kwenye mitandao na vyombo vya
habari. Mnawaaminisha mashabiki wenu kuwa mnapendana kwa kauli zenu
motomoto lakini ndani ya miezi miwili mitatu penzi chali.Wengine
mnaonesha kwamba mmedhamiria na kuamua kufunga ndoa kabisa, lakini
kumbe moyoni bado mnakuwa mna lenu jambo. Mashabiki wenu wanafurahia
kuona mmeoana lakini ndoa nayo haidumu, mnaachana.

Mbaya
zaidi mnapoachana mnapeana maneno ya kashfa, mnaumbuana kiasi ambacho
kinadhihirisha kabisa mlikuwa hamna mapenzi ya dhati au hamkudhamiria
kabisa kuingia kwenye ndoa.Hivi kama kweli mlipendana, nini
kinawafanya muanze kuumbuana? Badilikeni, mashabiki wenu wamechoka
kusikia kila kukicha ndoa ya staa fulani imevunjika, wachumba fulani
wameachana, ni aibu.
Watu hawapendi kuona Nay wa Mitego na Siwema mkiwa mmeachana. Tena
mnaachana kwa kupeana maneno yanayoonesha kwamba mlikuwa hamna nia ya
dhati ya kuwa wapenzi.Shamsa Ford na Dick, kapo yenu ilikuwa nzuri.
Mlipamba vyombo vya habari, uhusiano wenu ukazaa matunda ya mtoto
mmoja lakini ndoto ya kuishi kama mume na mke imeyeyuka.
Nasibu Abdul !٪Diamond!& na Wema Sepetu penzi lenu
lilikuwa likipendwa na wengi, likaishia njiani. Rose Ndauka na
Malick Bandawe mlioishi na kubahatika kupata mtoto mmoja, nini
kiliwakuta? Inasikitisha.Wolper na Dallas nao walipamba sana vyombo
vya habari lakini mwisho wa siku chali. Ndugu zangu, mnapaswa
kubadilika. Msiigize maisha yenu. Igizeni kwenye filamu, mkirudi
nyumbani mjitambue kwamba heshima, upendo, busara vinahitajika ili
kuishi na mwenzako.

Mbona
wapo wasanii wengi tu maarufu duniani na wamedumu kwenye uhusiano?
Kwa nini msiige mfano kwa mastaa kama Marlaw na mkewe, Jay Z na
Beyonce ambao wanaheshimu penzi lao hadi sasa?Jamani, cha msingi
mnapaswa kuheshimu suala la uhusiano, msifanye masihara katika maisha
ya ukweli. Vitu vingine vinapaswa kufanyika kwenye filamu pekee na
siyo kuvihamishia katika maisha halisi.
Bila shaka mtakuwa mmenielewa na mtabadilika, kila la kheri.