Dustan Shekidele, Morogoro.
SWADAKTA! Katika hali ya kustaajabisha, kijana mmoja aliyefahamika kwa
jina la Ramadhan, ambaye mwishoni mwa wiki amejikuta akishushiwa kipigo
kwa kudhaniwa kuwa kibaka, alisalimika baada ya kuanza kusali kwa
kuwashtakia kwa Mwenyezi Mungu waliokuwa wakimpiga, akisema hakuwa na
hatia na ghafla watu hao kusitisha kipigo.
Kijana Ramadhan akishusha dua zito baada ya kushushiwa kipigo kikali.
Ramadhan alikutana na hali hiyo baada ya kutuhumiwa kuiba redio kutoka katika duka moja lililopo stendi ya daladala mjini hapa.
Ilidaiwa kuwa kibaka huyo baada ya kuchukua redio hiyo alianza
kukimbia kutokana na mwenye duka kumwitia mwizi na Ramadhan akawa mmoja
kati ya watu waliokuwa wakimfukuza, kabla ya mdokozi huyo kujichanganya
na watu hivyo kutotambulika kirahisi.
Baada ya kuona hivyo, wananchi hao wenye hasira walimgeukia kijana
huyo na kuanza kumpa kipigo kama cha mbwa mwizi kwa vile nguo zake
zilikuwa zimefanana na zile zilizokuwa zimevaliwa na kibaka aliyekuwa
akifukuzwa.
....Akizidi kuomba.
”Ewe Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa msaada wako niepushie na
mtihani huu niliosingiziwa kwani wewe ndiwe unayejua ukweli wa tukio
hili,” mtu huyo alisikika akisema kufuatia kipigo alichokuwa akikipata,
baada ya kukimbia na kwenda kujibanza pembeni ya duka linalouza vinywaji
baridi.
Kufuatia maneno hayo, watu wote walijikuta wakisitisha zoezi la
kumpiga na mmoja wa bodaboda wa kijiwe cha Juwata aliingia kati na
kusema; “Jamani huyu jamaa anaonekana siyo mwizi na ni mtu wa dini,
hivyo naomba aliyeibiwa ajitokeze na kutoa ushuhuda,” alisema na hakuna
aliyejitokeza.
Baada ya kuona hivyo, kijana huyo aliwataka watu hao kumuacha aende
zake huku baadhi ya walioshiriki kumpiga wakimuomba msamaha mtu huyo
aliyekuwa akivuja damu mwili mzima.Akizungumza na mwandishi wetu,
Ramadhan alisema alishuka kwenye daladala na kuungana na watu waliokuwa
wakimfukuza mwizi kabla hawajamgeuzia kibao kutokana na nguo zake
kufanana na za kibaka.
Wananchi wenye hasira kali wakiwa eneo la tukio.
“Mwizi alijichanganya na watu ndipo nikageukiwa mimi, nikakimbilia
hapa dukani kwa Mhindi na kuamua kuomba msaada kwa Mungu kwa kuomba na
akafanikiwa kuniokoa,” alisema kijana huyo.
Katika stendi ya daladala, mfanyabiashara wa duka lililoibiwa,
aliyejitambulisha kwa jina la Shaaban, alisema alikuwa amekwenda
kutafuta chenchi, ndipo alipomuona mtu akiondoka na redio yake na yeye
akapiga kelele za mwizi, akadondosha bidhaa hiyo na kukimbia, lakini
akashindwa kuungana na watu kumkimbiza kwa vile hakukuwa na mtu mwingine
dukani