Mtoto baada ya kufanyiwa unyama huo.
Na Stephano Mango, SONGEA
MAJONZI! Bado ni tukio baya sana kutokea katika Kijiji cha
Kikunja, Kata ya Ndongosi, Wilaya ya Songea Vijijini mkoani Ruvuma
ambapo mkazi wa kijiji hicho, Amani Hyela (42), anadaiwa kuwaua kwa
kuwachinja kwa panga mpenzi wake, Ester na watoto wake wawili kisa
kikitajwa kuwa ni wivu wa mapenzi.
Tukio hilo la kutisha lilijiri saa saba usiku wa Novemba 28, mwaka
huu ambapo Amani anadaiwa kuwaua watu hao kwa kuwachinja na kuwakata na
panga sehemu mbalimbali za miili yao na baadaye yeye kujijeruhi kwa
kujikata shingoni na kujisababishia majeraha makubwa.
Kama ada ya Gazeti la Uwazi, mara baada ya kupata taarifa za ukatili
huo lilifika eneo la tukio na kujikusanyia maelezo kutoka kwa mashuhuda
na majirani wa eneo hilo.
“Mimi ni jirani wa marehemu Ester, siku hiyo usiku nilishtuliwa na
kelele za watu. Nikatoka nje na kubaini kuwa, kelele hizo zilikuwa
zikitokea kwenye nyumba hii. Kufika nikakuta watu wengi, mtuhumiwa yuko
chini anavuja damu.
“Niliulizia kulikoni, nikaambiwa Amani amevamia nyumbani hapo na
kumchinja Ester na watoto wake wote. Nilishangaa sana. Ester nilimwona
mchana wake, alikuwa wa afya njema kabisa. Huu ni ukatili. Dunia ya sasa
unyama umeongezeka sana. Si Tanzania tu. Kila mahali unyama, ukatili,”
alisema jirani mmoja aliyeomba hifadhi ya jina lake.
Mama akiwa amelala chini baada ya kufanyiwa kitendo hicho cha kinyama.
Shakira Moyo, mkazi wa kijiji hicho na mama mzazi wa marehemu Ester
aliliambia gazeti hili kuwa, ni unyama mkubwa ambao haujawahi kutokea
kwenye kijiji hicho na kwamba anamfahamu Amani ambaye ni mlalamikiwa.
Shakira alisema mauaji hayo yamemuumiza sana kwa vile yamempotezea
mwanaye na wajukuu wawili ambao kimsingi hawana hatia yoyote katika wivu
wa kimapenzi wa wazazi wao lakini wamekatishwa uhai wao.
Alisema kuwa marehemu Ester alikuwa na watoto wawili ambao walizaliwa
kwa baba tofauti (si Amani) lakini kwa kipindi cha miaka mitatu
iliyopita, Ester akawa na uhusiano wa kimapenzi na mwanaume huyo.
“Ester na Amani waliishi kama mume na mke na baadaye waliachana
kufuatia Ester kusema kuwa ameokoka na kwamba hataki tena masuala ya
mapenzi (nje ya ndoa) jambo ambalo lilipingwa na mwanaume,” alisema
Shakira.
Mtuhumiwa akiwa amefungwa kamba.
Aliongeza kuwa, kitendo hicho ndicho kilichomfanya Amani kuamua
kuchukua uamuzi huo uliosababisha vifo vya watu watatu na yeye mwenyewe
kujijeruhi ambapo pia alinusurika kifo kutoka kwa wananchi wenye hasira.
“Inaonekana Amani aliamini Ester anamkataa kwa kuwa ana mwanaume
mwingine ndiyo maana aliona bora amtoe uhai na kuwamaliza na watoto na
yeye ajiue. Naamini amejijeruhi lengo lilikuwa kujiua,” alisema mwanamke
huyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, ACP Mihayo Msikhela alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Alisema
siku ya tukio, baada ya taarifa kufika kituoni, polisi walikwenda eneo
husika na kukuta watu hao wameshafariki dunia huku mtuhumiwa akiwa
amejichinja koo akiwa amefungwa mikono kwa waya.
Alisema mtuhumiwa akiwa anavuja damu, alikimbizwa Hospitali ya Mkoa
wa Ruvuma ambako amelazwa akipatiwa matibabu huku akiwa chini ya ulinzi
mkali wa polisi.